The State University Of Zanzibar

Teknolojia kuinua upatikanaji elimu mjumuisho

Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Mhe. Leila Muhammed Mussa, amesemateknolojia ya kisasa  itaongeza kasi ya upatikanaji wa elimu  kwa watu wenye mahitaji maalum nchini.

Hayo aliyasema katika ufunguzi  wa semina ya siku  tatu iliyoanza leo tarehe 09/09/20024 katika Kampasi ya Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) huko Maruhubi. Katika semina hiyo ya  Kuondoa Vikwazo vya Elimu: Urekebishaji Mbinu Jumuishi  na Teknolojia katika Elimu Zanzibar alisema njia hii ya kisasa itabadilisha namna watu wenye ulemavu wanavyoweza kujipatia elimu kwa wepesi na kutatua changamoto zinazowakabili.

 ‘’Nimeridhishwa na kuona teknolojia inatumika katika ufundishaji kwa wanafunzi wenye ulemavu… tunaweza pia kuondosha pengo la upatikanaji wa elimu kwa kuimarisha utoaji wa elimu, na walimu kubuni  mazingira ya ufundidhaji,’’  alisema.

Aliongeza katika kuweka mazingira bora kwa watu wenye ulemavu, Serikali italazimika kubadilisha mtaala wa elimu ili kubadilisha mbinu za ufundishaji, kuwa na  miundombinu mahususi na kubadilisha mitazamo kwa wazazi kutambua namna ya kuishi na watu wenye mahitaji maalum.

Aidha, aliongeza kuwa mabadiliko yanayotarajiwa kufanyika yanapaswa kuwahusisha watu wote wakiwemo wanafunzi, walimu na wazazi kutambua namna gani waishi na watu wenye ulemavu.

Alifahamisha kuwa hakuna uwiano kati ya wanafunzi wanaosajiliwa kujiunga na masomo katika ngazi za msingi na sekondari ikilinganishwa na vyuo vikuu.

‘’Wanafunzi wenye ulemavu wanaojiunga vyuo vikuu ni wachache mno ikilinganishwa na waliosajiliwa  wanapoanza masomo, kila wakiendelea mbele wanapungua’’, alisisitiza.

Mapema, Makamo Mkuu wa SUZA, Prof. Mohd Makame Haji alisema kuwa  mchango wa wadau wa maendeleo  ni nyenzo muhimu katika kuimarisha maendeleo ya elimu yanayotakiwa Zanzibar.

Alisema kuwa maendeleo ya sera ya Elimu ya Zanzibar  yanayolenga kuondoa  vikwazo vya Elimu ni  ushuhuda wa utekelezaji wa jukumu hili.

Naye Balozi wa Finland nchini Tanzania Bi  Theresa Zitting akizungumza kwa njia ya mtandao alisema wana matarajio makubwa kwa mradi huu kutatua changamoto  za kielimu kwa watu wenye mahitaji maalum. 

Aidha, alikiri kiwango cha elimu kwa watu wenye mahitaji maalum kiwamgo cha elimu kwa watu wenye ulemavu kiko chini  hali inayochangiwa na kuwepo skuli chache  kwa watu wenye wahitaji maalum na watoto kutopelekwa  skuli. 

Mafunzo hayo yanawashirikisha  wadau mbali mbali  wakiwemo kutoka  taasisi zinazotoa mafunzo ya  elimu  mjumuisho,  vyuo vya  ualimu vya kati na mabaraza ya watu wenye ulemavu,  yameandaliwa kwa ushirikiano baina ya  SUZA na Chuo  Kikuu cha  Jamk cha Finland  na kuwashirikisha pia wanachama   walio kwenye mradi huo wakiwemo  Chuo Kikuu cha Ruanda na Chuo Kikuu cha Tempere cha Finland